ZANZIBAR-Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Mgeni Hassan Juma amesema,wakati umefika kwa wananchi kushirikiana na Serikali katika kudumisha Mila, Silka na Utamaduni wa Zanzibar ili kukuza Biashara ya Utalii.

Amesema, azma ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ni kuona vijana wanajiajiri na kukuza uchumi wa nchi yao kupitia Sanaa ya Utamaduni.
Aidha, amesema Zanzibar inategemea kwa kiasi kikubwa Biashara ya Utalii hivyo ni vyema kwa Wanajamii kuwaandaa Vijana wao ili waweze kuitumia Nyumba ya Sanaa kwa kupata Ujuzi.
Amesema maendeleo ya Sayansi na teknolojia, imepunguza nguvu ya Utamaduni wa Zanzibar lakini Serikali ya awamu ya 8, inachukuwa juhudi ya kurejesha Utamaduni huo wa asili.
Hata hivyo amewaomba Wazanzibar hususan Wasanii kurithibisha na kuitumia Sanaa kwa kudumisha Umoja, Mshikamano na kuitambulisha Zanzibar ndani na Nje ya Nchi.
Mkuu wa Wilaya ya Magharibi B, Hamida Mussa Khamis amesema kuwepo kwa Nyumba ya Sanaa ni hatua muhimu ya kuwasaidia Wananchi kupata ajira kupitia Sanaa mbalimbali, zilizopo hapa nchini.
Aidha, amesema mradi huo ni hatua muhimu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020-2025 katika kuimarisha na kujenga Miundombinu ya Sanaa Zanzibar.
Naye Kamishna wa Idara ya Sanaa Zanzibar Omar Salum Mohammed amesema, Ujenzi wa Nyumba ya Sanaa Zanzibar, unatarajiwa kuwa wa Ghorofa 3 na kugharimu zaidi ya Sh. Bilioni 3.
Nyumba hiyo ya Sanaa Mwanakwerekwe inataraijiwa kutoa mafunzo ya Fani mbalimbali ikiwemo ya Uchoraji, Uchongaji, Ushonaji, kudarizi na Ushoni.