DAR-Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Benki ya African Export-Import (AFREXIMBANK), Bw. Haytham ElMaayergi, ambapo wamejadili masuala mbalimbali yanayohusu uwekezaji katika viwanda vya kusindika mazao ya kilimo, sekta ya madini na utalii.
Katika kikao hicho kilichofanyika leo, tarehe 27 Januari 2025, katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam, Gavana Tutuba ameihimiza Benki ya AFREXIMBANK kuwekeza katika sekta ya madini nchini, hasa kwa kuwasaidia wachimbaji wadogo na wa kati wa dhahabu.
Ameeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza upatikanaji wa dhahabu, ambayo itanunuliwa na Benki Kuu na kuhifadhiwa kama sehemu ya akiba ya fedha za kigeni, hatua inayolenga kuimarisha uchumi wa taifa.