ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi ameeleza kuwa, ujenzi wa Skuli Unaofanywa na Serikali lengo lake ni Kuhakikisha Watoto wanapata fursa nzuri ya Elimu katika Mazingira Bora.
Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo alipoifungua Skuli Mpya ya Msingi ya Kojani wilaya ndogo ya Kojani Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Akizungumzia suala la ajira, Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi ameziagiza Wizara ya Afya,Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali na Utumishi kuhakikisha zjira zinapofanyika hususani Kojani ni lazima wapewe vijana wa kisiwa hicho na kuzitaka taasisi hizo kusimamia agizo hilo.
Agizo lingine amelitoa kwa Wizara ya Afya kupeleka Boti moja ya matibabu Kojani miongoni mwa Boti tano zilizoagizwa na wizara hiyo.
Halikadhalika Rais Dkt.Mwinyi amesisitiza kuwa,Serikali itaongeza wafanyakazi Kojani ili huduma ndogondogo katika nyanja mbalimbali zitolewe kisiwani.
Vilevile Rais Dkt.Mwinyi amewahakikishia wananchi kuwa Serikali inakusudia kutoa upendeleo maalum kwa ujenzi wa kiwanja cha kisasa cha michezo pamoja na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya kisiwani humo.
Ujenzi wa Skuli ya Msingi ya Kojani umegharimu shilingi bilioni 5.382 ikiwa na madarasa 32,maabara,chumba cha kompyuta, maktaba na ukumbi wa kufanyia mitihani na ina uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,305 kwa Mkondo Mmoja.