MWANZA-Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando Februari 5, 2025 imetembelewa na Madaktari Bingwa bobezi kutoka Hospitali ya Sahyadri iliyopo mjini pune - India waliofika kwa ajili ya Kambi ya matibabu ya kibingwa bobezi yanayohusisha magonjwa ya Pua, Koo,Masikio (ENT), ubongo, uti wa mgongo pamoja na mishipa ya fahamu katika Kliniki ya Madaktari Bingwa na Bingwa bobezi (Bugando Specialized polyclinic -Nera).
Akizungumza katika ujio wa Madaktari hao Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Bugando Dkt. Fabian A. Massaga amewakaribisha Madaktari hao katika kliniki ya Madaktari Bingwa na Bingwa bobezi ya Bugando Specialized polyclinic-Nera.
"Ni matumaini yetu kwamba kupitia kambi hii tutabadilishana ujuzi na kupeana uzoefu katika kazi kwani malengo yetu na nia zetu katika mashirikiano haya ni kusogeza huduma za kibingwa bobezi kwa wananchi kwa kutoa huduma zilizo boreka."
Dkt.Massaga ameendelea kueleza umuhimu wa mashirikiano haya kwa timu ya Madaktari wa Bungando kwani kupitia kambi hii tutajengeana uwezo wa hali ya juu katika utendaji kazi.
Naye Dkt. Samson Kichiba ambaye ni Meneja wa Kliniki ya Bugando amemshukuru Dkt. Massaga na uongozi mzima wa hospitali kwa kuendelea kusimama pamoja nao hata katika suala zima la mashirikiano.
"Tunaenda kuanza kambi hii kwa kushirikiana na Madaktari wa Sahyadri kuanzia Februari 6 hadi 9, 2025 ambapo tutafanya uchunguzi wa kina na upasuaji wa magonjwa ya koo, pua, masikio, ubongo pamoja na mishipa ya fahamu na ni matumaini yetu kwamba wagonjwa 200 wataenda kunufaika na kambi hii."