Dkt.Mpango aipongeza Jamhuri ya Korea kwa kuunga mkono miradi ya maendeleo Tanzania

DODOMA-Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania Mhe. Eunju Ahn, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma leo Februari 19,2025.
Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais amesema Tanzania inathamini na imedhamiria kuimarisha ushirikiano na Jamhuri ya Korea ulioanza tangu mwaka 1992 ambao unachagiza maendeleo katika sekta mbalimbali nchini.

Ameipongeza Jamhuri ya Korea kwa kuiunga mkono Tanzania katika sekta ya Elimu, Miundombinu, TEHAMA, Afya, Kilimo, Viwanda na Nishati.

Amesema makubaliano ya ushirikiano baina ya Tanzania na Korea katika madini ya kimkakati yataleta manufaa mengi zaidi kwa kuwa Tanzania imejaliwa kuwa na madini mengi ambayo yanaenda sambamba na mwelekeo wa dunia ya sasa ambayo inajikita katika uchumi wa teknolojia za kijani.

Aidha,Makamu wa Rais amemueleza Balozi wa Jamhuri ya Korea umuhimu wa kuongeza kiwango cha ufanyaji biashara baina ya Tanzania na Korea yenye manufaa kwa pande zote mbili.
Amesema ni muhimu wawekezaji na wafanyabiashara wa Korea kutembelea Tanzania mara kwa mara ili kujionea fursa zilizopo na kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda.

Amesema, uongezaji wa thamani kwa malighafi hapa hapa nchini utachochea biashara, uhamishaji teknolojia pamoja ongezeko la ajira kwa wananchi wa Tanzania.

Pia,Makamu wa Rais amesema Tanzania ipo tayari kushirikiana na Jamhuri ya Korea katika kubadilishana wafanyakazi, ambapo amemsihi Balozi huyo kuwezesha mchakato wa kujiunga katika Mfumo wa Vibali vya Ajira (EPS) ili wafanyakazi wa Tanzania waweze kuingia katika soko la ajira la Korea na kufanya kazi katika sekta mbalimbali kama vile ujenzi wa meli, sekta ya viwanda na kilimo cha kisasa.

Halikadhalika amesema ushirikiano unahitajika katika Elimu na kuwajengea uwezo wataalamu wa Afya kwa kuwapatia mafunzo katika ubingwa na ubobezi wa utoaji matibabu mbalimbali. Makamu wa Rais pia amesisitiza kushirikiana katika masuala ya utamaduni, michezo na lugha ya Kiswahili.
Kwa upande wake Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania Mhe. Eunju Ahn amesema katika kipindi atakachohudumu nafasi ya Ubalozi nchini Tanzania, atahakikisha anasimamia na kuharakisha kukamilika kwa makubaliano mbalimbali yaliyofikiwa baina ya Tanzania na Jamhuri ya Korea ikiwemo ushirikiano katika madini ya kimkakati na maendeleo ya uchumi wa buluu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news