Dkt.Mpango amuaga mama mzazi wa Waziri wa Elimu

KILIMANJARO-Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango na Mwenza wake Mama Mbonimpaye Mpango leo tarehe 06 Februari 2025, wameungana na viongozi na wananchi mbalimbali katika Ibada ya kumuaga marehemu Sekunda Massawe ambaye ni Mama mzazi wa Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda iliyofanyika katika Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Pius X - Tarakea mkoani Kilimanjaro.
Akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais amesema Serikali, inashukuru kwa maisha ya mama Sekunda ambaye alimzaa na kumlea Mhe. Prof. Adolf Mkenda, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia ambaye amekuwa Mtendaji na Kiongozi mahiri katika utumishi wa umma, tangu alipokuwa anafundisha Chuo Kikuu cha Dar es salaam na katika nafasi mbalimbali alizoshika Serikalini.
Amesema, Taifa linaendelea kufaidi matunda ya malezi bora na uchapakazi, ambayo mama Sekunda aliwapatia watoto wake. Ametoa rai kwa wazazi na walezi kufanya kila jitihada kusomesha watoto, kuwafundisha maadili mema, kushika dini yao kiadilifu, na kufanya kazi kwa bidii kwa faida yao wenyewe, familia na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema kila mmoja anapaswa kujitahidi kuishi vema na binadamu wenzake na kufanya kazi kwa bidii katika nafasi mbalimbali ili kutoa mchango mzuri kwa familia na Taifa, na kuacha historia nzuri na mifano bora ya kuigwa na jamii.

Ameongeza kwamba ni muhimu kujiandaa kumrudia Muumba maana hakuna ajuaye siku wala saa.
Ibada ya kumuaga marehemu Sekunda Massawe imeongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Moshi Mhashamu Ludovick Minde na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa, Wabunge, Viongozi wa Taasisi mbalimbali, Viongozi wa Dini pamoja na wananchi mbalimbali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news