BUJUMBURA-Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Tanzania itaanza kutoa huduma za matibabu ya ubingwa wa juu kwa wagonjwa nchini Burundi baada ya kukamilisha maandalizi ya kambi ya matibabu inayotegemewa kufanyika hivi karibuni.
Hatua hiyo imefikiwa katika ziara ya Wataalamu toka BMH wakiongozwa na Prof.Abel Makubi walipokutana na Uongozi wa Hospitali kuu za Prince Regent Charles na Gitega nchini Burundi chini ya uratibu wa Mhe. Gelasius Byakanwa, Balozi wa Tanzania nchini Burundi na Wizara ya Afya ya Burundi.
Mashirikiano haya yataruhusu BMH kufanya kambi za matibabu mbalimbali katika Hospitali ya Taifa mjini Bujumbura na pia ile ya Rufaa katika Mkoa wa Gitega na kwa wale wagonjwa ambao hawataweza kutibiwa nchini humo, watapata huduma katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dodoma.
Chini ya mpango, BMH pia itasaidia kutoa mafunzo ya ubingwa wa juu kwa watalaamu kutoka Burundi .