ARUSHA-Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imeshinda tuzo nane za TEHAMA zilizotolewa na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Tume ya TEHAMA, Soft Ventures, na TISPA kwa mwaka 2025. 

Tuzo hizo zimekabidhiwa Februari 21, 2025, jijini Arusha na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry Silaa kwa Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA kutoka TAMISEMI, Erick Kitali ambaye amepokea tuzo hizo kwa niaba ya Waziri wa Nchi, OR-TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa.
Akizungumza baada ya kupokea tuzo hizo, Kitali amesema mafanikio hayo yanatokana na uongozi imara na ubunifu katika matumizi ya TEHAMA kwa maendeleo ya Tanzania unaofanywa na serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mhe.Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan.
Ameongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yameendelea kuboreshwa kwa ubunifu na kuzingatia mahitaji ya watumiaji, huku yakijengwa kwa mawazo ya Kitanzania na ushirikiano madhubuti baina ya Wizara na taasisi nyingine za serikali.
TAMISEMI imeshinda nafasi ya kwanza kwa mifumo ya Tausi, M-Mama, na FFARS katika sekta za ushirikishwaji wa wananchi, afya, na fedha. Aidha, ilishinda nafasi ya pili na ya tatu kwa mifumo ya GOT-HOMIS, WEZESHA PORTAL, na Tausi katika vipengele mbalimbali.
Tuzo hizo zinalenga kuimarisha matumizi ya TEHAMA ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu wa kidijitali.