PWANI-Kaimu Katibu Tawala Mkoa ws Pwani, Shangwe Twamala amepokea ugeni kutoka Taasisi ya Kizimkazi Sport Promotion ya Zanzibar, ukiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu Furaha Hussein pamoja na timu kutoka DAR24 Media.
Ziara hiyo, iliyofanyika Februari 13, 2025, inalenga kushirikiana na serikali ya mkoa katika maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yatakayofanyika Machi 8, 2025, wilayani Mkuranga.
Katika kuelekea maadhimisho hayo, taasisi hiyo inapanga kutoa misaada kwa wanawake, ikiwemo khanga, pedi, sabuni, pampers, na mikoba ya kliniki kwa wajawazito na wanawake waliopo hospitalini.
Pia, wanatarajia kupanda miti ya matunda ili kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha upatikanaji wa lishe bora. Shughuli nyingine zitakazofanyika ni pamoja na mbio za taratibu, usafi katika hospitali, na mikutano na wananchi.