SONGWE-Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe limemkamata mwanaume mmoja ambaye ni raia wa Malawi kwa tuhuma za kupatikana na nyara za Serikali.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi,SACP Augustino Senga amesema tukio hill limetokea Februari 16, 2025 saa 04:30 usiku huko Kitongoji cha Msia Kata ya Chitete, Tarafa ya Bulambya Wilaya ya Ileje Mkoa wa Songwe.
Amesema,Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe kupitia taarifa za kiintelijensia pamoja na misako na doria za mara kwa mara zinazoendelea kufanyika ikiwa ni pamoja na kushirikiana na idara mbalimbali ikwemo Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Wilaya ya Ileje limefanikiwa kumkamata Chisamba Siame Kameme (60) raia wa Malawi akiwa na vipande 18 vya meno ya tembo yenye uzito wa kilo 84.2.
Kamanda huyo amesema, baada ya kufanya tathimini na wataalam ilionesha kuwa thamani ya meno hayo ni shilingi milioni 153.540,000 ikiwa ni sawa na tembo watatu.
Amesema, kila tembo mmoja ana thamani ya shilingi milioni 51.2 ambapo alikuwa ameviweka kwenye mfuko wa salfeti kisha kufunga kwenye baiskeli rangi nyeusi kwa lengo la kuviuza.
Pia, amesema upelelezi bado unaendelea na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria huku akiwataka wenye tabia za kufanya uhalifu kuacha mara moja.