ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dkt.Hussein Ali Mwinyi amewaongoza viongozi mbalimbali na wananchi katika Dua Maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Ali Hassan Mwinyi.
Dua hiyo imefanyika Mangapwani Zawiani kijijini kwao na mahala alipozikwa Hayati Mzee Mwinyi, Wilaya ya Kaskazini A, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Hayati Ali Hassan Mwinyi alifariki Februari 29,2024 katika Hospitali ya Mzena jijini Dar es Salaam alipokuwa akitibiwa akiwa na miaka 99.
Akizungumza katika dua hiyo,Rais wa Zanzibar Alhaj Dkt.Mwinyi ametoa shukrani kwa watu wote walioshiriki dua hiyo,kwani wameonesha jinsi wanavyoendelea kumuenzi Mzee Mwinyi na kuwasihi kuendelea kumuombea.
Wakati huo huo Alhaj Dkt.Mwinyi ameufungua Msikiti Mpya wa Ali Hassan Mwinyi uliojengwa kijijini hapo na kuwashukuru wahisani waliojenga msikiti huo marehemu Zakaria na familia yake.