Wataalamu Sekta ya Utalii watakiwa kuleta maboresho katika sekta hiyo

NA HAPPINESS SHAYO

WATENDAJI na Maafisa Utalii nchini wametakiwa kufanya kazi kwa uadilifu, kujituma na ubunifu kuhakikisha Sekta ya Utalii inaboreshwa kwa manufaa ya Taifa.
Hayo yamesemwa leo Februari 22, 2025 na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi, Dkt. Pindi Chana (Mb) katika Kikao kazi cha wataalamu wa Utalii na Masoko kutoka Idara ya Utalii , Wizara ya Maliasili na Utalii na Bodi ya Utalii kilichofanyika jijini Tanga.

"Nitoe wito kwa washiriki wote wa mafunzo haya kutumia fursa hii adhimu kuhakikisha tunajifunza na kuja na mikakati madhubuti ya kuboresha Sekta ya utalii nchini," amesisitiza Mhe. Chana.

Aidha, ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha nia ya kuleta mageuzi katika sekta hiyo kupitia programu ya Tanzania the Royal Tour na Amazing Tanzania.
"Kwa mara ya kwanza sekta hii imevunja rekodi kwa kufikia watalii 5,360,247 ambapo idadi ya watalii wa Kimataifa imefikia 2,141,895 na watalii wa ndani ni 3,218,352 na mapato yatokanayo na shughuli za utalii yalifikia dola za Marekani bilioni 3.9,"amesema Mhe. Chana.

Awali, akimkaribisha Waziri wa Maliasili na Utalii, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dunstan Kitandula aliwataka maafisa Utalii kuyajua mazingira ya maeneo yao ya kazi ili kutoa huduma bora kwa wananchi na watalii wanaotembelea maeneo hayo.
Mhe. Kitandula alisema kuwa Maafisa Utalii wanatakiwa kujua mahitaji ya wateja wanaowahudumia ili kuongeza fursa za wateja kurudi tena kutalii.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt.Hassan Abbasi amesema lengo la mkutano huo ni kuongezeana ujuzi wa namna ya kutangaza kidigitali na kuongeza mazao mapya ya utalii.

Kikao hicho kilichohudhuriwa na baadhi ya Watendaji na Maafisa Utalii na Masoko kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kiliambatana na mafunzo ikiwemo masuala ya afya ya akili, kutumia mbinu za kisasa katika masoko ya kidijitali na matumizi ya akili mnemba (Al).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news