DAR-Klabu ya Yanga SC imemtangaza Miloud Hamdi mwenye uraia wa Algeria na Ufaransa kuwa kocha wake mpya akichukua mikoba ya Sead Ramovic ambaye anaondoka klabuni hapo baada ya kuvunja mkataba na kocha Mjerumani huyo kwa makubaliano ya pande zote mbili.
Taarifa ya leo Februari 04, 2025 iliyotolewa na klabu hiyo imebainisha kuwa, Kocha Hamdi mwenye uzoefu mkubwa wa kufundisha soka akiwa amefanya kazi barani Ulaya, Asia na Afrika, anaungana na timu mara moja kuanza majukumu yake mapya.
Kocha huyo mbali na uzoefu alionao, pia ana mafanikio makubwa katika soka la Afrika akishinda taji la Ligi Kuu ya Algeria na kucheza Fainali ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika msimu wa 2015-2016 akiwa na USM Alger.