DAR-Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limemkamata Elia Asule Mbugi maarufu Dogo Bata (25) Mkazi wa Segerea ambaye ni dereva aliyekuwa akiendesha gari namba T 580 EAE aina TATA (daladala) ambaye alitoroka Machi 17, 2025.
Ni baada ya kusababisha ajali iliyosababisha kifo cha SP Awadh Ramadhani Chico aliyekuwa Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi Chanika jijini Dar es Salaam.

SACP Muliro amesema mtuhumiwa huyo alikamatwa na Makachero wa Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam Machi 27, 2025 huko maeneo ya Mbalizi mkoani Mbeya na atafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo.
OCD Chico alifariki Machi 17,2025 katika ajali ya gari akiwa anaelekea kazini katika barabara ya 33 Nyerere maeneo ya Pugu mwisho wa lami, baada ya gari lake kugongana na daladala ambapo alizikwa March 18, 2025 katika makaburi ya Kisutu Ilala jijini Dar es salaam.