NA DIRAMAKINI
GAVANA wa Jimbo la Warrap nchini Sudan Kusini, Jenerali Magok Magok Deng ameibua mjadala mzito katika jimbo hilo baada ya kumfukuza kazi Kamishna wa Mamlaka ya Mapato (State Revenues Authority-SRA), Abraham Makuek ikiwa ni siku 18 tangu ateuliwe.
Kwa mujibu wa Juba Eye, katika kukoleza mafuta kwenye moto, Gavana Magok amemteua mtoto wake Deng Mangok (Deng Mariel) kushikilia nafasi hiyo ya Kamishna wa Mapato.
Uamuzi huo umezusha mijadala mizito ndani na nje ya jimbo hilo huku wengi wakihoji kuhusu uwazi na haki katika uteuzi huo.
Gavana Magok ambaye aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Sudan Kusini, Mheshimiwa Salva Kiir hivi karibuni, alimchagua Makuek kuongoza State Revenues Authority (SRA).
Ingawa, uamuzi huo umezua maswali mengi kutoka kwa wanasiasa, wachambuzi na wakazi wa Jimbo la Warrap, ambao wamebaki kwenye mshangao wa hatua hiyo.
Pia, uamuzi huo umetajwa kuwa na viashiria vya ukabila na upendeleo huku wengi wakisema uteuzi wa Deng Mangok hautakuwa na matokeo mazuri serikalini.
Kwa sasa, Gavana Magok anasubiriwa kutoa ufafanuzi wa kutosha kuhusu uamuzi huo, lengo likiwa ni kulinda na kuyapa maslahi ya Taifa na Jimbo la Warrap kipaumbele.
Warrap ni kati ya majimbo 10 ya Sudan Kusini na ndipo himaya Rais Salva Kiir (alizaliwa huko). Pia, ndipo ngome walipozaliwa majenerali na wanasiasa wengi maarufu nchini humo akiwemo Akol Koor Kuc.