DAR-Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Richard Lyimo amesema, hayuko tayari kuungana na vyama vingine vya siasa vya upinzani katika Uchaguzi Mkuu ujao kama chama chake hakitapewa nafasi ya kutoa mgombea wa urais.
Lyimo ameweka wazi hayo jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na wanahabari waliofika ofisini kwake kwa lengo la kutaka kujua kama chama chake kitakuwa sehemu ya kuungana na kwa lengo la nguvu ya pamoja katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu.
“Kama watataka tuungane nitawaeleza kwamba wakipe nafasi chama changu kitoe mgombea wa urais na si vinginevyo na ikiwa watakubali hakutakuwa na shida ila hatuwezi kuingia kwenye mtego wa kufanya chama kingine kiwe kikubwa.
“Ebu angalia Chama Cha Wananchi (CUF), marehemu Maalim Seif Sharif Hamad wakati ule aliingia kwenye UKAWA angalia kilichotokea, CUF hii si ile kwani wakati wanaingia katika muunganiko huo hawakuangalia ruzuku itakuwawaje,” amesema.
Amefafanua kwamba,chama siku zote kinajengwa na ruzuku hivyo unapoungana unafanya kimoja kiwe kikubwa kutokana na kusikika katika uchaguzi huo na vinaweza kupata idadi kubwa ya wabunge, madiwani na vingine vififia na kuvinyanyua ni kazi kubwa kwa maana kuviendesha inahitaji ruzuku.
Pia alisema wakati wa UKAWA, Wenyeviti wa Chama walikubaliana wasiingiliwe katika majimbo yao, ingawa cha kushangaza mmojawapo aliwekewa mgombea kwenye jimbo lake kitu ambacho alifafanua kilikuwa kinyume cha makubaliano.
Lyimo anaamini kwamba muungano huo ambao tayari baadhi ya viongozi wa vyama upinzani wameanza kuugusia wakiamini ndio mwarobaini wa kuking’oa Chama Cha Mapinduzi (CCM), madarakani kwenye Uchaguz Mkuu ujao, anasema mchakato huo utaishia njiani na ni kama sehemu ya kuwaongopea Watanzania.