Kamati ya Bunge yaridhishwa na ujenzi wa jengo la TBC Dodoma

DODOMA-Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Husna Sekiboko imeridhishwa na ujenzi wa mradi wa Ofisi Mpya za Makao Makuu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) unaotekelezwa katika Mtaa wa Vikonje Kata ya Mtumba Wilaya ya Dodoma mkoani Dodoma.
Kamati hiyo imetembelea na kukagua mradi huo Machi 12, 2025 ambapo ujenzi huo utafanyika kwa awamu nne na unatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 53.7 hadi kukamilika. 

Aidha, awamu ya kwanza ya mradi huo imefikia asilimia 45 na inatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 2025.
Ujenzi wa awamu ya kwanza unahusisha jengo la utawala, studio za redio, televisheni, mitandao ya kijamii, pamoja na usimikaji wa mitambo yote muhimu ya uandaaji na urushaji wa matangazo, ikiwemo satellite uplink, transmission studio, na server-based system.
TBC inatekeleza maelekezo ya kuhamia Dodoma ili kutimiza azma ya muda mrefu ya Serikali ya kuhamishia Makao Makuu ya nchi Dodoma. Kwa mujibu wa mipango iliyopo, ifikapo mwaka 2026, studio zote zitakuwa zimekamilika, mitambo itakuwa imesimikwa, na shughuli rasmi za utangazaji wa redio, televisheni, na mitandao ya kijamii zitafanyika jijini Dodoma, yakiwa ni Makao Makuu ya Shirika.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news