Tanzania na UNOPS zaendelea kuimarisha ushirikiano katika miradi ya maendeleo

DAR-Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel William Shelukindo, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Ofisi za Umoja wa Mataifa za Huduma za Miradi (UNOPS), Bw. Rainer Frauenfeld, aliyefuatana na ujumbe wake.
Katika mazungumzo hayo, Balozi Shelukindo amepongeza ushirikiano mzuri kati ya Serikali ya Tanzania na UNOPS katika kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.

Amesisitiza kuwa, Tanzania inathamini mchango wa UNOPS katika sekta mbalimbali, hususan miundombinu ya barabara na huduma za kijamii, ambazo zimekuwa na mchango mkubwa katika kuinua uchumi wa Taifa na kuboresha maisha ya wananchi.
Aidha, Balozi Shelukindo ameweka bayana dhamira ya Serikali kuendelea kushirikiana na UNOPS ili kuhakikisha miradi inayotekelezwa inazidi kuleta tija na kuendana na vipaumbele vya maendeleo vya Taifa.

Pia, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya utekelezaji wa miradi kwa ufanisi zaidi ili kuhakikisha malengo yaliyokusudiwa yanafikiwa kwa wakati.

Kwa upande wake, Bw. Frauenfeld ameipongeza Tanzania kwa kuwa moja ya nchi zinazotekeleza vyema vipaumbele vya Umoja wa Mataifa, hususan katika kuboresha huduma za kijamii.
Aidha, amesisitiza azma ya UNOPS kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo.

Katika hatua muhimu ya kuimarisha ushirikiano huu, UNOPS imefungua rasmi ofisi yake nchini Tanzania. 

Hatua hii inalenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kurahisisha usimamizi wa shughuli zake, na kuimarisha ushirikiano wa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine wa maendeleo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news