DODOMA-Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Duniani (WMD) Machi 23, 2025 kwa kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na kusheherekea miaka 75 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).

Katika siku hiyo, Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Mwakiposa Kihenzile alitoa ujumbe kwa umma akimwakilisha Waziri wa Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa na kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa kutoa huduma bora.
“Katika Siku hii ya Hali ya Hewa Duniani, Serikali inapongeza kazi nzuri inayofanywa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika utoaji wa huduma za hali ya hewa zilizoboreshwa sana, ikiwa ni pamoja na utoaji wa tahadhari wakati wa matukio ya hali mbaya ya hewa,”alisema Mhe. Kihenzile.
Mhe. Kihenzile alieleza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha huduma za hali ya hewa kwa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa zaidi na kuendelea kuwajengea uwezo wataalamu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt. Ladslaus Chang’a amesema Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania imechukua hatua za kimkakati kupitia teknolojia za kisasa kama akili mnemba (AI) kuboresha utabiri na tahadhari za hali mbaya ya hewa.
Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Kwa Pamoja Tushughulikie Pengo la Utoaji wa Tahadhari”.
Tags
Habari
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)
Siku ya Hali ya Hewa Duniani
Tanzania Meteorological Agency (TMA)