ZANZIBAR-Kamisheni ya Utalii Zanzibar (ZCT) imesaini mkataba wa ushirikiano na Klabu ya Yanga SC kwa ajili ya kuitangaza Zanzibar kupitia kampeni ya “Visit Zanzibar” kwa msimu wa 2025/2026. Nembo ya kampeni hiyo itaonekana kwenye jezi rasmi za Yanga katika mashindano yote.

Akizungumzia kuhusu hatua hiyo,Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, Mhe. Mudrick Ramadhan Soraga amesema;
"Niwapongeze sana Viongozi wa Young Africans SC chini ya Rais wake,Mhandisi Hersi Said kwa ushirikiano mkubwa mlioutoa kutoka mwanzo mpaka leo tunapokwenda kusaini mahusiano haya ya ushirikiano wa kutangaza Utalii wa Zanzibar.
"Sekta ya Utalii ina ushindani mkubwa sana, licha ya jina kubwa tulilokuwa nalo bado tunapata ushindani sana kutoka katika Visiwa vya jirani hivyo ni lazima kama Wizara tuweke nguvu kubwa kwenye kujitangaza.
"Niseme wazi kama kuna Taasisi bora yenye nguvu na ushawishi ambayo tungeweza kufanya nayo kazi kutusaidia kwenye suala hili la kutangaza vivutio vyetu vya Utalii hapa Zanzibar, basi namba moja na sahihi kwa sasa ni Klabu ya Young Africans SC,"amesema Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar Mhe. Mudrick Ramadhan Soraga.
Kwa upande wake, Rais wa Young Africans Sports Club (Yanga SC), Mhandisi Hersi Said amesema kuwa;
"Tunafuraha kubwa kupata fursa hii ya kuingia mahusiano ya ushirikiano na Kamisheni ya Utalii chini ya Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kwa ajili ya kutangaza vivutio vya Utalii hapa Zanzibar.

"Young Africans SC tunaitazama Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kama jicho la Zanzibar, mahusiano tunayoingia leo ni kwa ajili ya kuutangaza utalii wa Zanzibar kupitia Klabu yetu.
"Na mahusiano haya sio kutangaza tu bali kutoa elimu na uelewa juu ya vivutio vyote vya utalii Zanzibar,"amesema Rais wa Young Africans SC,Mhandisi Hersi Said.