Gavana Tutuba afanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya VISA

WASHINGTON-Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Emmanuel Tutuba amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya VISA anayesimamia Ukanda wa Ulaya ya Kati, Mashariki ya Kati na Afrika, Bw. Andrew Torre.
Katika kikao hicho, viongozi hao walijadili kwa kina namna mbalimbali za kupunguza gharama za miamala ya kifedha, kudhibiti uhalifu wa kimtandao, na kuimarisha utoaji wa elimu ya fedha kwa wananchi.
Masuala hayo yanalenga kupunguza matumizi ya fedha taslimu pamoja na kuongeza upatikanaji na matumizi ya huduma rasmi za kifedha, hasa zile zinazotolewa kwa njia ya kidigitali.
Aidha, kampuni ya VISA ilieleza dhamira yake ya kuendelea kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania kwa kutoa mafunzo na kubadilishana ujuzi wa kitaalamu, ili kuimarisha mifumo ya malipo kuwa salama, rahisi na jumuishi kwa Watanzania wote.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, Mkurugenzi wa Utafiti na Sera za Uchumi BoT, Dkt. Suleiman Missango, Meneja wa Sera ya Fedha BoT, Bi. Asimwe Bashagi, pamoja na maafisa waandamizi kutoka kampuni ya VISA.
Mazungumzo hayo yamefanyika sambamba na Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya IMF na Benki ya Dunia, inayoendelea jijini Washington D.C., Marekani.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news