DODOMA-Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka mabalozi kuiishi falsafa ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha mahusiano na kukuza diplomasia ya kiuchumi kati ya Tanzania na mataifa mbalimbali duniani.

Ameyasema hayo leolJumapili, Aprili 6, 2025 alipokutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Balozi Hamad Khamis Hamad Balozi wa Tanzania nchini Msumbuji na Mheshimiwa Balozi Holmes Matinyi, Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Ofisini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma.
Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali ina mategemeo makubwa na mabalozi hao, hivyo wanapaswa kwenda kuendeleza mahusiano mazuri ya muda mrefu yaliyopo baina ya Tanzania na mataifa hayo.
Waziri Mkuu amesema pamoja na mambo mengine mabalozi hao wanatakiwa wahakikishe wanasimamia vizuri matumizi ya fedha katika ofisi zao pamoja na kuanzisha au kuendeleza madarasa ya kufundisha lugha ya kiswahili.